Inaonyesha machapisho yaliyo na lebo MAHUSIANO. Onyesha machapisho yote
Inaonyesha machapisho yaliyo na lebo MAHUSIANO. Onyesha machapisho yote

Ijumaa, 24 Februari 2017

Bwana Yesu asifiwe mpendwa msomaji! Tumsifu Yesu Kristo!
Naamini unaendelea vizuri katika kujenga Ufalme wa Mungu hapa duniani..Na ninaamini unaendelea kujitakasa katika Bwana ili ajapo kulichukua 'kanisa lake takatifu' na wewe uwemo, haleluya!
Ndugu msomaji napenda kukushirikisha jambo hili muhimu la NDOA katika kizazi hiki. Ukitazama makanisani, katika jamii, maofisini,n.k. suala la migogoro ya ndoa limekuwa jambo la kawaida. Siku hizi hata "watu wale wa njia hii" nao kuachana au kupeana talaka limekuwa jambo la kawaida sana. Wakati umefika ambapo kila aliye wa Bwana ijulikane! Tumesahau kuwa sisi wa Ulimwengu huu, na shetani amepofusha wanandoa kwa kuwa hawazijui nafasi ambazo Mungu amewapa ili waweze kutimiza kusudi lake jema! Ukifuatilia Biblia kwa msaada wa Roho Mtakatifu, utagundua kuwa suala la NDOA mwanamke amepewa nafasi zake na mwanaume amepewa nafasi zake kiroho ili kuhakikisha ndoa inatimiza kusudi lake. Leo napenda nikushirikishe nafasi mojawapo ya mwanamke katika ndoa. Kibiblia mwanamke amepewa nafasi (positions) nyingi za kumsaidia kuimarisha NDOA YAKE. Nafasi hizo ni kama ifuatavyo:

Mwanamke kama Mjenzi kwa mumewe
Mwanamke kama Msaidizi
Mwanamke kama Mleta Kibari kwa mumewe
Mwanamke kama Mshauri wa mumewe
Mwanamke kama Mlinzi kwa mumewe n.k.

Ndugu msomaji, unajua kuwa mwanamke akisimama kwenye nafasi yake amepewa "mamlaka" ya kujenga ndoa yake? 
Hebu tusome (Mithali 14:1) kwa pamoja. 
"Kila mwanamke aliye na "hekima" hujenga nyumba yake;Bali aliye "mpumbavu" huibomoa kwa mikono yake mwenyewe".
Haleluya! Biblia inasema, "mke mwenye hekima ndiye anayejenga nyumba yake, tena kwa mikono yake mwenyewe. Lakini pia inasema, mke mpumbavu anbomoa nyumba yake...Neno "nyumba" linaashiria "familia" au "ndoa". Sikia mtu wa Mungu, mwanamke amepewa nafasi au wadhifa katika ulimwengu wa Roho kujenga nyumba yake au ndoa yake au familia yake. Hii haimaanishi 'baba' hana nafasi katika ndoa yake, hapana; isipokuwa katika somo hili nazungumzia mwanamke (woman). Ikiwa kina mama wataamua kukaa katika nafasi zao, ukweli ni kwamba ndoa zitapona. Kanisa litaimarika, utukufu apewe Yesu Kristo! "mpumbavu" ni mtu yule anayejua anachopaswa kufanya lakini hafanyi. Biblia haisemi "mwanamke aliye mjinga" bali "aliye mpumbavu". Sikia mama neno hili ambalo Roho anakukumbusha, keti katika nafasi yako katika ndoa yako, na nafasi mojawapo ni KUIJENGA NYUMBA YAKO, kumbuka kuwa kama kuna suala la kujenga, uwe na uhakika, si suala la siku moja, bali ni suala la kila mara panapotokea ufa.
NB: Huwezi kujenga nyumba ambayo imekamilika, bali unajenga nyumba ambayo haijakamilika. Hivyo hekima yako inahitajika mama hasa pale "ndoa yako inapokuwa katika changamoto" ili ujenge mahali penye nyufa. 

Mambo unayopaswa kuzingatia ili uweze kujenga nyumba yako (ndoa yako).

1. Utiifu kwa mumeo
Sikia ewe mwanamke, maandiko yanatuambia kuwa; mnapaswa kuwatii waume zenu kama kumtii Bwana.
Ukisoma Waefeso 5:22, "Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu".
Ili mwanamke aweze kujenga nyumba yake hana budi kumtii mumewe, tena amtii kama vile anavyomtii Bwana Yesu wetu Kristo. Hili si jambo dogo, ni jukumu kubwa lakini lenye baraka na ushindi kwenye ndoa na Ufalme wa Mungu. Kwa nini siku hizi kina mama walio wengi hawataki kuwatii waume zao? Wanategemea kweli ndoa zao zikae salama wakati mioyo yao imejaa dharau, kiburi na visasi visivyoisha? Ndivyo neno la Bwana linavyotufundisha? Sikia mwanamke jambo hili, haijalishi mumeo anakufanyia vituko gani, ikiwa kweli Bwana Yesu ni tegemeo lako, hutajaa dharau na kiburi kwa mumeo. Wewe unachopaswa kufanya ni kuonyesha kuwa unamtii tena kama kumtii Bwana wetu Yesu. Soma 1Petro 3:1. "Kadhalika ninyi wake, watiini waume zenu; kusudi, ikiwa wako wasioliamini Neno, wavutwe kwa mwenendo wa wake zao, pasipo lile Neno".
Umeona mwanamke unapokuwa mtiifu kwa mumeo kinachotokea? Maandiko yanasema, "mwenendo wa mke ukiwa vizuri; unaweza kumvuta hata mume asiyeamini, halelujah! Mume wako akigundua unamtii toka moyoni mwako pasipo unafiki, nakueleza ukweli, utashangaa kitakachotokea. "Utii wako ni mbinu mojawapo ya kuijenga ndoa yako mama. Usikubali Ibilisi akudanganye na hila zake, wewe mtii mume wako. Kumbuka kuwa "usipomtii mumeo" unatenda dhambi. Utaniuliza kwa nini? Kwa sababu "dhambi ni uasi"(1Yohana 3:4). Kwa lugha nyingine, unaasi maagizo ya Mungu katika neno lake la kuwa "umtii mume wako". Maandiko hayasemi umtii mume anayemwamini Bwana wetu, bali hata kama hamchi Mungu wewe "mtii tu". Mungu akutie nguvu katika Kristo Yesu kwa njia ya Roho Mtakatifu ili akupe nguvu na hekima uweze kujenga ndoa yako. Biblia inasema, "Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu (Wafilip 4:13). Sikia mwanamke, hata wewe unayaweza mambo yote katika yeye akutiaye nguvu.

2. Kutunza siri za mume wako.
Je, huwa unatunza siri za mumeo ewe mwanamke? Kwa nini hufanyi hivyo? Miongoni mwa vitu ambavyo Ibilisi anatumia ni "kina mama kumpa nafasi katika kutoa siri za waume zao nje wakidhani watasifiwa au kusaidiwa. Sikia mama na uelewe, haijalishi mumeo ana mapungufu kiasi gani, usiyatoe nje, yatunze kwani huo ni udhaifu tu wa mumeo. Usitumie udhaifu wake kumpiga nyundo kichwani, bali tumia udhaifu wake kumjenga na kumuombea. Sijaesema kuwa usitafute msaada kwa wapendwa, hapana, ila Roho akuongoze kwa mtu ambaye ana hekima ya Mungu, bali si kila mtu unamueleza mambo ya ndoa yako, linda kinywa chako uwe na siri. Narudia tena, tunza siri za mume wako hata kama anakutesa. Sisi si wa ulimwengu huu, na wewe si wa ulimwengu huu, hivyo, mienendo ya ulimwengu huu haikuhusu (Yohana 17:16). 
Ukisoma "Tito 2:3-5), neno la Mungu linasema hivi:
"....ili wawatie wanawake vijana akili, wawapende waume zao, na kuwapenda watoto wao, na kuwa wenye kiasi, kuwa safi, kufanya kazi nyumbani mwao, kuwa wema, kuwatii waume zao wenyewe; ili neno la Mungu lisitukanwe"
Nataka uone hili neno, "kuwa wenye kiasi" "self-control" . Sikia mwanamke, jitahidi usiseme mambo ya ndoa yako, maandiko yanasema, uwe na kiasi katika uyatendayo yakiwemo na ya mumeo. Unafikiri unapopeleka siri za mumeo nje unamsaidia? La hasha! humsaidii bali unatoa nfasi kwa shetani ili aweze kuwavuruga. Mpende mumeo na umuombee....Be self-controlled in all you do. 

3. Matumizi ya kinywa chako
Miongoni mwa viiungo Ibilisi anavitumia kuangamiza watoto wa Nuru ni 'vinywa vyao' au maneno ya vinywa vyao yasiyo na uzima ndani yao wanayoyatamka juu ya waume zao bila kujua madhara yake. Hebu tusome (Mithali 18:7-8). "Kinywa cha mpumbavu ni uharibifu wake mwenyewe, na midomo yake ni mtego wa nafsi yake". Maandiko yanasema, maneno yanayotoka kinywani mwa mpumbavu huharibu nafsi yake, na maneno hayo ni mtego wa nafsi yake. Jizuie usimnenee mumeo maneno mabaya, kwani yeye (mume) ni kichwa chako. Tusome pia "Zaburi 36:4, Huwaza maovu kitandani pake, hujiweka katika njia mbaya; ubaya hauchukii". Ukisoma kwa makini mstari huu, utaona jambo hili. Mpumbavu anaponena bila utaratibu hujiweka katika njia ya uangamivu, na mtu wa namna hii hachukii hata ubaya. Kumbuka jambo hili, kuna roho za giza ambazo zinafuatilia maneno unayosema juu ya mumeo ili yaumbike na unashangaa yanampata. Mungu amekupa nafasi uzitumie kujenga na si kubomoa. Haijalishi mumeo yukoje, wewe mnenee mema kila wakati. Laiti watu wangejua uharibu unaotokana na maneno ya vinywa vyao, naamini wangelinda sana maneno yawatokayo. ukisoma (Mithali 12:14a "Mtu atashiba mema kwa matunda ya kinywa chake.....
Siku zote mtu hujazwa na yale asemayo kutoka kinywani mwake. UKISOMA Mithali 12:22a, "Midomo ya uongo ni chukizo kwa BWANA......Ukisoma ule mstari wa 18, Biblia inasema, kuna kunena bila kufikiri....Jitahidi kabla hujanena ufikiri unachotaka kusema juu ya nyumba yako au ndoa yako. Acha umbeya wewe si wa ulimwengu huu (Yohana 17:16), tena ya kale yamepita sasa yamekuwa mapya (2Kor 5:17). Soma Mithali 13:3, "Yeye alindaye kinywa chake huilinda nafsi yake; Bali afunuaye midomo yake atapata uharibifu. Linda kinywa chako mama ili uilinde nafsi yako na uepuke uharibifu. Ombea kinywa chako na ukikabidhi kwa Bwana ili kitumike kama silaha ya haki.

4. MSAMAHA
Biblia inasema, kabla mtu hajaomba hana budi kwanza kusamehe waliomkosea. Marko 11:25, 26. "Nanyi kila msimamapo na kusali, SAMEHENI MKIWA NA NENO JUU YA MTU; ili na Baba yenu aliye mbinguni AWASAMEHE ninyi makosa yenu. Lakini kama ninyi hamsamehi, wala Baba yenu aliye mbinguni HATAWASAMEHE ninyi makosa yenu". 
Mungu atusamehe wapendwa, eneo hili ni la muhimu sana. Mimi naamini kuwa, mtu akiweza kuwa na roho ya kusamehe; huyo atashinda vikwazo vingi na atakuwa na AFYA NAFSINI mwake siku zote. Ukisoma hayo maneno juu utaelewa jambo hili: Ukitaka maombi yako yasikilizwe na Baba yetu wa Mbinguni ni lazima "tuwasamehe" waliotukosea. Lakini pia, tusipowasamehe, tunatenda dhambi kwa sababu tumeasi maagizo ya Mungu. Na dhambi ni uasi 1Yohana 3:4. Hivyo huwezi kuitwa tena mwana wa Mungu. Ukisoma hii mistari vizuri, haisemi tuwasamehe wakituomba msamaha la hasha! Tunatakiwa kusamehe bila kuombwa msamaha. Wanawake wengi siku hizi za mwisho, atakuambia; "nimemsamehe mpaka nimechoka". Unakumbuka wanafunzi wa Yesu walivyomuuliza Yesu "mtu anikose mara ngapi nami nimsamehe? Hata mara saba? Yesu aliwajibu sikuambii hata mara saba bali hata saba mara sabini...wanafunzi wakamjibu, Bwana tuongezee imani. Hivyo, Yesu alikuwa anawafundisha kuwa, wasamehe hata bila kuombwa msamaha. Haijalishi unakosewa mara ngapi kwa siku wewe samehe. Kibaya zaidi, wake pasipo kujua nao wanalipa visasi dhidi ya waume zao. Usilipe kisasi ewe mwanamke, kisasi ni cha Bwana yeye atalipa. Mume wako akikosea wewe mbebe kwenye maombi. Najua utanimbia, "nimeomba mpaka nimechoka, ni sawa kwa jinsi ya kibinadamu; lakini kwa jinsi ya Rohoni, hutakiwi kuchoka. Soma (Yakobo 5:10-18, Mathayo 5:14).
Ufanye nini ili usamehe mume wako? Fanya yafuatayo:
Moja: Fahamu kuwa si wewe bali Kristo aliye ndani yako. Wagalatia 2:20. Ukifanyiwa mabaya hufanyiwi wewe bali Kristo aliye ndani yako.Mume wako akikutukana; wewe linda kinywa chako huku ukijua kuwa hutukanwi wewe bali Yesu aliye ndani yako. Ukipigwa, usirudishe bali fahamu kuwa anafanyiwa hayo Yesu aliye ndani yako. Kusameheana hakupo siku hizi kati ya wanandoa, kwani upendo wa wengi umekwishapoa. 

Pili: Mpende mume wako (adui yako) na umuombee.
Mathayo 5:43, 44. MMesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako na umchukie adui yako; Lakini mimi (Yesu) nawaambia, wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi. Jizoeze kumuombea mume wako anapokuudhi. Tena mpende hata akikufanyia ubaya. Kumbuka kila wakati jambo hili muhimu, hakuna msamaha wa kweli pasipo upendo. Yohana 3:16.
 Watu wengi wanafanya kile Yesu alichowaambia wasifanye..Yesu alisema "wapendeni adui zenu".Kama adui unatakiwa umpende, kwa nini unamchukia mume wako? Katika watu wa Mungu, chuki imejaa na hii imeharibu ndoa nyingi. Biblia inasema, tuwapende wale wanaotuudhi. Kwa nini Yesu alisema tuwapende wale wanaotuudhi? Ni ili tupate kuwa wana wa Baba yetu (Mungu) Mathayo 5:45-47.ukisoma 1kor 13:4-8, utakuta tabia za upendo wa watu wa nuru. utakuta uvumilivu, kustahimili yote, kuamini yote, upendo haupungui wakati wowote, hufadhili, hautakabari, hauhesabu mabaya, hauoni uchungu n.k. 
 
Tatu:  samehe na kusahau
Ukisoma 'Luka 17:4, 5.  Maandiko yanatuambia, ...hata saba mara sabini, maana yake hata usipoombwa msamaha wewe samehe. Kusamehe ni uamuzi wa mara moja lakini kusahau ni vita vya imani. Ngoja nikuulize swali, Je! siku ulipookoka ulikuwa na uhakika gani kuwa umesamehewa dhambi zako na wala Mungu hazikumbuki tena? Lakini je, unaona kuwa Mungu anaweza kukuambia ufanye kitu aambacho anajua huwezi kufanya? Kumbuka ukimsamehe mume wako, usikumbuke tena hayo na usiyaweke moyoni. Msamehe bila unafiki ndani yake. Haleluya! haleluya! Tunayaweza mambo yote....Wafilipi 4:13. Soma pia Yakobo 4:7, Waefeso 4:27, Wafilipi 4:8. Kumbuka unasamehe kwa ajili yako mwenyewe.

Nne:Peleka hasira kwenye maombi
"Mwe na hasira, ila msitende dhambi jua lisichwe na uchungu wenu bado haujawatoka; wala msimpe Ibilisi nafasi" (Waefeso 4:26-27). Huu mstari wa "mwe na hasira ila msitende dhambi" watu wameutumia isivyo. Kutokana na maneno hayo wamefanya vitendo vingi viovu kwa mawazo, maneno na kwa matendo. Biblia haiwezi kujipinga yenyewe. Roho Mtakatifu ndiye aliyewaongoza watu kuandika maandiko hayo matakatifu. Lakini, soma mistari ifuatayo: 
"Uchungu wote na gadhabu na HASIRA na kelele na matukano YAONDOKE KWENU" (Waefeso 4:31). 
.....HASIRA ya mwanadamu haitendi haki ya Mungu" (Yakobo 1:20).
"Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya HASIRA na watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu (Wagalatia 5:19-21). Hapa unaona jinsi hasira inavyofananishwa na uchawi, uasherati, uadui, ibada ya sanamu, na mambo mengi yanayofanana na hayo.
Ukisoma (Mathayo 5:21, 22), Yesu akikaza ubaya wa hasira alisema "Mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, Usiue; na mtu akiua, itampasa hukumu. Bali mimi nawaambieni, kila amwoneaye ndugu yake HASIRA itampasa HUKUMU". Yesu anasema ukimuonea ndugu yako hasira unastahili hukumu...lakini Roho aliyema ndani ya Paulo ni huyo huyo aliyesema ndani ya Yesu. Tukirudi kwa Paulo, maandiko yanasema, ikitokea ukakasirika kwa sababu ya maudhi, jitahidi usitende dhambi. Maadamu tupo chini ya jua, hatutaweza kukwepa kukasirika, lakini Roho anasema kuwa "tukikasirika tusitende dhambi". Hivyo kuwa na hasira ni dhambi, ndiyo maana Yesu anasema, ukimwonea hasira ndugu yako (mume wako) unastahili hukumu, yaani umefananishwa na muuaji, mwasherati, mwabudu sanamu na mambo kama hayo. Swali linakuja, ikiwa umekasirika ufanyeje? Nakushauri katika Roho wa Mungu, fanya yafuatayo...
1. Kwana tubu kwa Baba juu ya kukasirika kwako
2. Pili, mwambie Baba jinsi unavyojisikia moyoni mwako bila kumficha kitu.
3. Tatu mwombe kitu ambacho ungependa akufanyie, utajikuta unaumimina moyo wako kwa Bwana naye ataichukua hasira yako na uchungu uliokuwa nao. Na badala yake anahuisha upya upendo ndani ya moyo wako. Ukiona bado hasira inakusumbua "ikemee kwa jina la Yesu nayo itatoka. Kosa la wengi wakiudhiwa wanapeleka uchungu na hasira kwa aliyewaudhi, sivyo biblia inavyoagiza, wewe upeleke kwenye kwa Yesu kwa njia ya maombi.

Tano: FURAHI SIKU ZOTE
Siri ya ushindi katika matatizo yoyote inatokana na furaha ya Bwana ndani yetu. Furaha ya Bwana ndiyo nguvu zetu. Wafilip 4:4;Furahini katika Bwana siku zote, tena nasema, Furahini. 
Ndugu msomaji Bwana na akubariki, akupe macho ya ndani uone kile anachotaka ukione, hakuna ndoa isiyo na mapungufu, lakini Yesu alitununua ili tujenge boma, na wewe mwanamke, tumia nafasi hii ya KUJENGA ili ujenge ndoa yako. Kumbuka iko mikononi mwako. Mungu awabariki, nawatakia Jumamosi njema.             

 

NAFASI YA MWANAMKE KATIKA NDOA YAKE KIBIBLIA

Jumapili, 19 Februari 2017

Mpendwa msomaji wa VIPAUMBELE KWANZA
Bwana Yesu asifiwe! Tumsifu Yesu Kristo!
Ni matumaini yangu kuwa umeamka salama kabisa, ni jambo la kumshukuru Mungu wetu katika Kristo Yesu! Ni neema na rehema tumepewa, si kwamba tunastahili, la hasha!
Ndugu msomaji wa makala hii, ningekushauri kabla ya kusoma ujumbe huu uombe uongozi wa Roho Mtakatifu ili uweze kupata kilichomo ndani yake. Tukumbuke kuwa hakuna anayejua kila kitu katika maandiko matakatifu (BIBLIA) bali tunapewa kwa sehemu (1 Wakor 13:9) "Kwa maana tunafahamu kwa sehemu; na tunafanya unabii kwa sehemu).
Ndugu msomaji katika vitu ambavyo kwa kasi vinazidi kupoteza "kusudi la kuumbwa kwake ni MISINGI YA NDOA KIBIBLIA, na hii hutokana na hila za yule adui yetu Shetani anazoingiza katika ndoa kwa njia nyingi sana. Anaingiza misingi na mtazamo wa kwake wa giza kupitia elimu, mila na desturi za watu na mpaka yapo baadhi ya madhehebu yameanza kupotosha misingi ya ndoa kibiblia.
 Ikiwa kweli tunataka kuponya ndoa zetu ipasavyo, hatuna budi kuifahamu kweli ya neno la Mungu katika eneo la ndoa na kuitii na si vinginevyo (Yohana 8:32) "Tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru, ukisoma ule mstari wa 36 unaongeza hivi: Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kwelikweli. Haleluya!
Ndiyo maana Biblia inasema " Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa" (Hosea 4:6b) 
 Ukisoma vizuri huo mstari maandiko hayasemi watu wa dunia hii, bali watu wa Mungu (waliookoka ndio wanaoangamizwa), wanaangamizwa kwa sababu gani? Hawaangamizwi kwa kuwa wana dhambi, hapana! Wanaangamizwa kwa kukosa MAARIFA ya neno la Mungu. Si kwamba hawaombi, wanaomba! Si kwamba hawahudhurii ibada za Jumapili au Jumamosi hapana! Neno la Mungu linasema, wamekosa maarifa yatokanayo na neno lake (Mungu). Fahamu hili: Tukijua sana; tunaweza sana. 

Ndugu mpendwa msomaji, turudi kwenye somo letu.
Naamini wote tunafahamu kuwa kila kilicho hai na kisicho hai vimeumbwa na Mungu, kama huamini, Mungu akusaidie na akutie nuru macho yako ya ndani uone sawasawa. Kwa sababu hiyo, hata NDOA imeanzishwa na Mungu kwa kusudi fulani la Ufalme wake. Katika makala hii sitazungumzia kusudi la ndoa, bali nitazungumzia MTAZAMO tunaopaswa kuwa nao juu ya NDOA kibiblia. Ukisoma (Mwanzo 2:24), maandiko yanasema hivi: " Kwa hiyo mwanaume atamwacha baba yake na mama yake (wazazi) naye (mwanaume) ataambatana na mkewe, nao watakuwa MWILI MMOJA).Bwana Yesu asifiwe!
Ndoa ni muunganiko wa watu wawili (mwanaume na mwanamke) na kuishi pamoja kama mume na mke. Hili neno nao watakuwa mwili mmoja huwa linanipa maswali mengi sana!
Kwa nini najiuliza hivi? kwa sababu wakioana bado utaona miili miwili, si ndiyo mpendwa msomaji? Lakini wakati natafakari jambo hili, liliingia wazo ndani yangu hivi:
Kwani Biblia inaposema, "Mungu ni mmoja inamaanisha nini? Mungu ni mmoja lakini katika nafsi tatu (Holy Trinity). Mungu Baba, Mungu Mwana na Mungu Roho Mtakatifu. Yesu alisema, "Mimi ni ndani ya baba na Baba yu ndani yangu. Lakini pia ukisoma (Waefeso 5:31-33) utakuta uhusiano wa mke na mume umefananishwa na uhusiano wa kanisa na Kristo Yesu. Yesu Kristo apewe sifa! Biblia inasema na "na hao wawili watakuwa mwili mmoja), kumbe nilifahamu ghafla moyoni mwangu kuwa, moyo wako na moyo wa mke wako vimeambatana, hivyo huwezi kutenganisha moyo wa mke na moyo wa mume. Biblia inaposema tuwe ndani ya Kristo na Kristo awe ndani yetu, haimaanishi tuingie na mwili wa nyama, hapana bali mioyo yetu iko kwake, HALELUYA!
Pointi ya kwanza nayotaka uifahamu ni hii" ILI NDOA IWE HAI LAZIMA MOYO WA MKE NA MUME VIAMBATANE. Na ili viambatane, inabidi mwanamke afanye jambo hili;
AWASAHAU WATU WA NYUMBANI KWAKE , YAANI HUKO KWA WAZAZI WAKE. Kwa lugha nyingine nafasi waliyokuwa nayo watu wa nyumbani kwao, aipe mume ili sasa waambatane.i.e. Kipaumbele cha mume kiwe cha kwanza baada ya Yesu moyoni mwake. Hebu soma (Zaburi 45:10-11). "Sikia binti utazame utege sikio lako. Uwasahau watu wako na nyumba ya baba yako na mfalme (mume) atautamani uzuri wako, maana ndiye akupaye bwana wako naye umsujudie. Praise the LORD JESUS!

point ya pili: Mke na mume wanapaswa kuwa na sura ya Mungu ndani yao.
Biblia inasema, "Mwanzo 1:26", Mungu akasema, Na tumfanye mtu kwa sura yetu....mstari wa 27, ...'Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba....
Ukisoma maandiko vizuri utafahamu kuwa, Mungu ni Roho (Yohana 4:24), hivyo hazungungumzii sura ya kimwili, bali sura ya rohoni. Ukiwa na Yesu, una sura ya Mungu kwa kuwa Yesu ni sura ya Mungu. Hivyo, ukiwa na Yesu, vipaumbele vyako vyote vinatanguliza kwanza Ufalme wa Mungu. Na shetani anajua kuwa ukipoteza mtazamo wa kimungu juu ya ndoa moyoni mwako (in your soul), umepoteza sura ya Mungu ndani yako, na hivyo ndoa inaanza kupoteza mwelekeo, na kinachofuata ni kifo cha kiroho (mauti), yaani kutengwa na uwepo wa Mungu. Hivyo ukiwa na sura ya Mungu unakuwa na uwepo wa Mungu, Yesu anakuongoza kwa njia ya Roho Mtakatifu namna ya kuendesha ndoa yako na mambo mengine.

Pointi ya tatu: Hekima ya kujenga nyumba au ndoa amepewa mwanamke na si mwanaume!
Simaanishi kuwa, mwanaume hana umuhimu katika ndoa yake la hasha! Biblia isingesema, mume ni kichwa cha mkewe kama vile Kristo alivyo Kichwa cha kanisa! Nazungumzia nafasi ya mwanamke kwa mumewe. Soma Mithali 14:1, "Mwanamke mwenye hekima huijenga nyumba yake....tukumbuke kuwa, Mwanzo 1:26-28, Mwanamke na mwanaume wameumbwa kwa sura ya Mungu, hivyo mke mwenye sura ya Mungu ana hekima ya kuijenga ndoa yake, sura ya Mungu ikipotea ndani yake, mauti inatawala ndoa, yaani wanatengwa na uso wa Mungu na wanaanza kwenda bila utaratibu wa Kimungu, na mwisho wao ni shetani kuwaangamiza (Hosea 4:6a). Mwanamke amepewa nafasi nyingi juu ya ndoa yake kibiblia. Amepewa nafasi kama vile
  1.     Mjenzi
  2. Mleta kibali kwa mumewe
  3. Mshauri
      4.Msaidizi 
Zipo nafasi nyingi sana alizopewa mke; tutaziangalia katika somo litakalofuata kwa undani zaidi.
Ndugu msomaji, napenda nikuambie jambo zito, kama hatutamgeukia Bwana Yesu na kumkaribisha katika ndoa zetu, hakika hatutaona ushindi. Lakini pia ni muhimu tuifahamu kweli ya neno lake juu ya kuwepon kwa ndoa ndipo tutakuwa huru kwelikweli. Inashangaza siku hizi kuona watu wakipewa chumvi ya kutembea nayo ili ilinde ndoa zao. Sikatai inaweza ikatokea Mungu akatumia chumvi, lakini sio formula ya maisha. Hakuna mtaalamu wa ndoa zaidi ya Bwana Yesu kukaa katikati ya ndao mwenyewe na kujawa na maarifa ya kiuungu ndani yetu. Siku hizi ni za mwisho, wale tulioamua kumtumikia Mungu katika Kristo Yesu tumtumikie kama apendavyo.

Pointi ya nne: Mke ni kiumbe dhaifu hivyo mwanaume anapaswa kuishi naye kwa kwa akili.
Ukisoma 1Petro 3:7 unasema hivi: "Kadhalika ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe"
Wakati najifunza juu ya mstari huu nilijiuliza maswali mengi sana, nayo ni hya:
1. Biblia imesema mwanamke mwenye hekima huijenga nyumba yake, je! huu udhaifu umetoka wapi tena?
2. Je! huu udhaifu unaosemwa ni udhaifu upi, wa kiroho au wa kimwili au ni upi? Nilijiuliza sana ikabidi nisome biblia ya Kiingereza na kilugha ili kuweza kuelewa anachotaka Mungu tuelewe. Nikasoma NEW INTERNATIONAL VERSION (NIV) 1Peter 3:7), panasomeka hivi:
"Husbands, in the same way be considerate as you live with your wives, and treat them with respect as the weaker partner and as heirs with you of the gracious gift of life, so that nothing will hinder your prayers.
Bwana Yesu tusaidie hatua kwa hatua jambo hili:
Jambo la kwanza: Biblia inatushauri kukaa na wake zetu kwa akili , ukisoma kwa kingereza anasema "be considerate" ghafla nikaanza kuelewa maana yake nini, considerate imetokana na neno consider, na neno consider   linamaanisha heed, think critically, or pay attention. Nikaanza kupata picha kuwa, considerate humaanisha "be attentive", "be mindful", "be thoughtful", "be careful not to cause harm to others", glory to Jesus!
Hivyo neno ishi na mke wako kwa akili maana yake: 'In whatever you do to your wife, before you do it, be careful not to cause harm to your wife or Be thoughtful when you treat your partner. Maana yake, Jihadhari unapotenda jambo kwa mke wako, lisiwe na madhara kwake kiroho na kimwili.Kwa lugha nyingine, kwa kuwa mke ni dhaifu, ndivyo ameumbwa, chochote unachotaka kutenda kifikiri ikiwa hakina madhara kwake, kwa nini kwa sababu mke anapenda umfanyie mambo anayotaka kwa kumjali, muonyeshe kuwa yeye ni wa thamani kwako. Treat them with respect....let she know that you really value her. 
Hebu tusome haya maaandiko kutoka kitabu cha J.B.PHILLIPS COPYRIGHT. 
Panasomeka hivi " Similary, you husbands should try to understand the wives you live with, honouring them as physically weaker yet equally heirs with you of the grace of eternal life. If you do not do this, you will find it impossible to pray properly"
Hapa anasisitiza hivi: ...try to understand the wives you live with...Maana yake , jitahidi kumuelewa mke wako: Kumuelewaje? Tuchukue mfano: Umetoka kazini ukakuta "mama hayupo, unashangaa anarudi muda ambao hukuzoea, je unachukua maamuzi gani? Kumbuka Biblia inasema, "mke ni dhaifu" nadhani hasira siku zote ni mbaya, lakini ukifuatilia Mungu anachotufundisha hapa utafahamu haraka kuwa " akifika jitahidi kwanza kumpa nafasi ajieleze na unapomjibu Mungu akusaidie usiwe na uchungu naye, maamuzi utakayochukua yasiharibu uhusiano wenu na Mungu, lakini pia yasilete madhara (hurt) kwa mke wako. Kama vile unavyoongea na mtoto mdogo, hivyo hivyo ongea na mke wako. Ukweli ni kwamba tukiwakasirikia hawa wake zetu, tutawaua, kiukweli ni wadhaifu. Tuwatendee kwa upole na kwa utulivu. 
Najua si jambo lepesi, lakini maandiko yanasema " nayaweza yote katika yeye atutiaye nguvu. Hata wewe unaweza. Mheshimu mke wako, jitahidi kumsikiliza kwa upole na kwa umakini huku ukijitahidi kumuonyesha kuwa unamjali. Akili ya mwanamke inahitaji kusikilizwa na kueleweka. Tujitahidi tusiwe na uchungu nao. Tutaangalia somo hili hatua kwa hatua. Naomba uniombee kwa kadri uwezavyo, Yesu akubariki!    
 

MUNGU NDIYE MWANZILISHI WA NDOA

Alhamisi, 26 Januari 2017


UMEKWAMISHWA NA NINI RAFIKI?